Skip to main content

UNENE UNAKUSUMBUA?



Iwapo unene unakusumbua kitu cha kwanza unachotakiwa kutambua ni kwamba mwili wako unahifadhi kiasi kikubwa cha mafuta kutokana na lishe yako kuliko kile kinachotumiwa na mwili huo kama chanzo cha nishati ya kuendeshea shughuli mbalimbali katika seli za mwili.

Unapojikuta kwenye mazingira ya aina hii, ni vizuri ukatambua kuwa kuna haja ya kubadili mwelekeo wako kuhusu mambo kadhaa, na hususan lishe. Mabadiliko katika lishe ni lazima yajumuishe kanuni zifuatazo:

1. Kuachana kwa kiasi kikubwa na vyakula ambavyo baada ya kuchakatuliwa ndani ya mwili vinazalisha kiwango kingi sana cha nishati (calories);

2. Kuongeza ulaji wa vyakula ambavyo vinatumia nishati nyingi sana kuchakatuliwa ukilinganisha na kiasi cha nishati inayoongezwa mwilini na vyakula husika;

3. Kuhakikisha umeshiba kiasi cha kuridhisha na hususan nyakati za mchana;

4. Kuongeza kwenye chakula chako viungo vinavyojulikana kwa uwezo wake wa kuchochea kasi ya uundwaji na uvunjifu wa kemikali mwilini (Spices that boost metabolism); na

5. Ongeza kiasi cha maji unachokunywa.

VYAKULA VINAVYOZALISHA WINGI WA NISHATI

Vyakula vyote vya wanga, na hususan vile vya nafaka (ukiondoa mboga za majani) huzalisha kiwango kikubwa cha nishati ndani ya mwili.
Nishati hii inapozidi kiwango kinachohitajika kwa matumizi ya mwili kiasi kilichobaki hugeuzwa kuwa mafuta na kuhifadhiwa mwilini kwa ajili ya matumizi ya baadaye. 

Katika uhalisia ni mara chache sana kupatikana mazingira ya kuwezesha matumizi haya ya baadaye na nishati, hivyo basi mhusika atajikuta akiendelea kulundika mafuta mwilini kutokana na lishe ya wanga anaokula mara kwa mara. 

Vyakula vya wanga vilivyochakatuliwa (processed) ni vibaya zaidi kuliko vile ambavyo ni vizima (unprocessed). 

Hii nikutokana na ukweli kwamba vyakula ambavyo havijachakatuliwa vinajumuisha pia kiasi kikubwa cha nyuzi lishe (fibers), madini, vimeng'enyo, vitamini, nakadhalika. 

Vitu hivi siyo tu kwamba vinasababisha kiwango halisi cha wanga kuwa kidogo, lakini pia ni virutubisho muhimu vinavyochangia katika kuboresha afya ya mwili kwa ujumla.

VYAKULA VINAVYOTUMIA NISHATI NYINGI

Baadhi ya vyakula, hususan baadhi ya protini, mathalani nyama, huhitaji kiasi kikubwa sana cha nishati kuandaliwa mwilini kabla ya virutubisho vilivyomo kufyonzwa mwilini. 

Kiasi hiki cha nishati ni kikubwa sana ukilinganisha na kile kitakachoingizwa na vyakula hivi ndani ya mwili. 

Matokeo yake ni kwamba badala ya mwili kuhifadhi mafuta, unaunguza mafuta yaliyohifadhiwa mwilini ili kutoa nishati ya ziada inayohitajiwa na mchakato wa kuchakatua vyakula husika pale vinapokuwa vimeliwa.

KUHAKIKISHA UMESHIBA

Katika mambo ambayo ni ajabu kabisa ni kwamba mwili wako hauwezi kuunguza mafuta yaliyohifadhiwa iwapo hukushiba!

 Homoni inayotoa ishara kwa mwili kuanza kuunguza mafuta inaitwa LEPTIN; homoni hii huzalishwa tu na mwili pale unapokuwa umeshiba. 

Njia nzuri sana ya kuifanya homoni hii kufanya kazi kwa ufanisi ni kula ushibe vyakula ambavyo havina kiwanga kikubwa cha wanga ndani yake.

 Hii ina maana kuwa LEPTIN itakayozalishwa itatoa ishara kwa mwili kuchoma mafuta yaliyohifadhiwa, bila vyakula ulivyokula kukuongezea kiwango kikubwa cha nishati mwilini kitakachopelekea kuwe na hitajio la kuhifadhi kiasi ambacho hakihitajiwi na mwili kwa wakati huo. 

Chakula bora kabisa kitakachojaza tumbo lako na wakati huohuo kukuongezea hazina luluki ya virutubisho, bila kukupa kitisho cha kukuongezea nishati ni MBOGA ZA MAJANI.

 Jitahidi 80% ya nafasi kwenye sahani yako iwe imejazwa na mboga za majani, na ikiwezekana sehemu kubwa ya mboga hizi iwe ni mbichi. Kama lengo ni kupunguza uzito, basi 20% iliyobaki ijazwe na protini (nususan nyama) na mafuta bora kama nazi au siagi.

VIUNGO

Baadhi ya viungo vina sifa ya kuongeza kasi ya mchakato wa ujenzi na uvunjifu wa kemikali mwilini. 

Wataalamu wanasema kasi ya uvunjifu na ujenzi wa kemikali mwilini inapoongezeka, basi na kasi ya mwili kuchoma mafuta huongezeka pia. Mdalasini na pilipili hutajwa kuwa baadhi ya viungo ambavyo ni bora sana kwa ajili ya kazi hiyo.

MAJI YA KUNYWA

Baadhi ya watafiti wanayataja maji kuwa na umuhimu mkubwa sana katika suala la kudhibiti ongezeko la mwili. 

Mwili unapopungukiwa maji, utaratibu wa mgawo wa maji ndani ya mwili unazinduliwa.

 Katika utaratibu huu baadhi ya shughuli za mwili husitishwa au kupunguzwa kasi yake katika jitihada za kudhibiti kiasi kidogo cha maji kilichopo.

 Usitishaji huu wa baadhi ya shughuli, au upunguzaji kasi wake moja kwa moja hupunguza kasi ya uvunjifu au ujenzi wa kemikali mwilini, na hivyo kupunguza kasi ya uunguzaji wa mafuta yaliyohifadhiwa ndani ya mwili. 

TAHADHARI.

 Ni hatari kusubiri mpaka usikie kiu ndiyo unywe maji. Mpaka ukisikia kiu basi ujue kuwa tayari ushakabiliwa na upungufu mkubwa wa maji ndani ya mwili, na tayari viungo vya mwili wako vishaanza kukumbwa na athari hasi.
 Hii ni kwa sababu HISIA YA KIU (thirsty sensation) hupungua kadri umri unavyoongezeka. 

Ni kawaida kwa watu wazima kupata upungufu mkubwa wa maji bila wao wenyewe kujijua. Maji ni dawa, hivyo basi tuyanywe kama hivyo na siyo vinginevyo. Mtu mzima unahitaji kiasi cha lita tatu kwa siku.

                 CREDIT  :   HERBAL IMPACT

Comments